window.__reverb = {}; window.__reverb.__reverbLoadedPromise = new Promise((resolve, reject) => { window.__reverb.__resolveReverbLoaded = resolve; window.__reverb.__rejectReverbLoaded = reject; }); window.__reverb.__reverbTimeout = setTimeout(() => { window.__reverb.__rejectReverbLoaded(); }, 5000);

Ukraine yazishambulia na kuziteketeza ndege 40 za kivita za Urusi

Ukraine inadai kuzipiga takriban ndege 40 za Urusi 40, katika kile kinachoonekana kuwa moja ya mashambulizi makali zaidi hadi sasa kwenye anga za Urusi.

Muhtasari

  • Zelensky alisimamia mashambulizi dhidi ya vituo vya ndege vya Urusi, vyanzo vya usalama vya Ukraine vyasema
  • Shambulio kubwa la Ukraine nchini Urusi: Tunachojua kufikia sasa
  • Urusi yadai hujuma huku afisa mkuu wa jeshi la Ukraine akijiuzulu
  • Ukraine yazishambulia na kuziteketeza ndege 40 za kivita za Urusi
  • Hamas yatoa hakikisho la kuwaachilia mateka ila inataka mabadiliko kufanywa kwenye mpango wa kusitisha vita Gaza unaosimaiwa na Marekani
  • Raila Odinga 'Walipeni fidia jamaa za waliofariki kwenye maandamano ya Gen Z 2024'
  • Mwanaharakati nchini Kenya azuiliwa kwa kubuni mtandao wa kupinga mswada wa fedha wa 2025
  • Mamia wakamatwa kwenye ghasia zilizotokea Paris baada ya ushindi wa PSG wa klabu
  • Watu saba wafariki baada ya madaraja mawili ya Urusi kuporomoka
  • Wakenya washerehekea sikukuu ya Madaraka Day
  • Watu 26 wafariki baada ya vifaru vya Israel kushambulia Gaza - waokoaji

Moja kwa moja

Abdalla Seif na Leila Mohammed

  1. Jinsi Ukraine ilivyotekeleza shambulizi dhidi ya ndege 40 za Urusi

    .

    Chanzo cha picha, Source in the SBU

    Kwa mujibu wa vyanzo ndani ya kitengo cha SBU vilivyozungumza na idhaa ya Ukraine ya BBC, maelezo ya ziada jinsi kitengo hicho maalum cha Ukraine kilivyopanga na kutekeleza shambulizi la kutumia ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi za jeshi la angani la Urusi.

    Kulingana na SBU, kutokana na shambulizi hilo kwenye kambi hizo nne za jeshi la angani, ndege muhumi 41 za kivita za Urusi ziliharibiwa.

    Mamlaka nchini Urusi zimethibitisha kwamba ndege zisizo na rubani zilishambulia maeneo ambayo kambi mbili za jeshi la angani zipo, ila hawajazungumzia hasara iliyopatikana hasa kwenye ndege za kivita.

    Vyanzo ndani ya SBU vimesema kwamba , operehsni iliyotekelezwa mapema leo, ilipangwa kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja unusu, na kusimamiwa kibinafsi na Rais wa Ukraine Volodomyr Zelensky na kutekelezwa na mkuu wa usalama nchini Ukraine Vasyl Malyuk na wahudumu wa majukumu maalum.

    Aidha vyanzo hivyo ndani ya SBU vimethibitisha kwamba ndege zisizo na rubani kutoka Ukraine zilikuwa zikipaa angani kutoka kwa malori ambayo yaliendeshwa hadi nje ya kambi hizo za kijeshi.

    “SBU ilituma ndege hizo zisizo na rubani za aina ya FPV hadi Urusi, na kisha baadae kutuma nyumba za mbao ambazo zinaweza kusafirhishwa,” ripoti hiyo ilisema.”

    Baadaye, zilipowasili katika himaya ya Urusi, ndege hizo zilifichwa chini ya paa za nyumba hizo ambazo zilikuwa zimewekwa juu ya Malori.

    Na wakati mwafaka ulipofika, paa za nyumba hizi zilifunguliwa kwa mbali na ndege hizo kulenga silaha za kurusha makombora za Urusi.”

    Wakati huo huo, vyanzo vingine vya SBU vimedai kwamba “walioshiriki katika shambulizi hilo maalum ya kijeshi wamekuwa Ukraine kwa muda mrefu sana.”

    Idhaa ya Ukraine ya BBC pia imepata picha za wakati ambapo ndege hizo zilipotekeleza shambulizi hilo.

    Kwa misingi ya hali ya vita hivi, BBC haiwezi kuthibitisha uzito wa taarifa kutoka kwa maafisa wa serikali ya mataifa hayo mawili.

  2. Habari za hivi punde, Urusi yamkamata dereva wa gari lililohusika na mashambulizi ya droni

    Mamlaka ya Urusi inamshikilia dereva wa lori anayedhaniwa kuhusika katika shambulio la ndege za kivita .

    Chombo cha habari kinachoendeshwa na serikali ya Urusi Tass kimeripoti kuwa dereva wa lori linaloaminika kuhusika na shambulio hilo la ndege zisizo na rubani atahojiwa na polisi.

    Ripoti hiyo inaongeza zaidi kuwa "idadi kamili ya ndege zisizo na rubani za UAV bado hazijahesabiwa", lakini inasema hakuna tishio kwa umma kwa wakati huu.

  3. Zelensky alisimamia mashambulizi dhidi ya vituo vya ndege vya Urusi - Vyanzo

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Taarifa za kustaajabisha na za kina kuhusu shambulizi la mapema leo nchini Urusi zimetolewa kwa vyombo vya Habari kisiri.

    Taarifa hizo zinatoa maelezo zaidi kuhusu jinsi jeshi la Ukraine lilivyopanga na kutekeleza shambulizi dhidi ya kambi nne za jeshi la angani la Urusi.

    Kwa mujibu wa vyanzo ndani ya huduma ya usalama ya Ukraine (SBU) , Operesheni hiyo iliyotambuliwa kama Spider Web ilichukuwa mwaka mzima na nusu kupanga na ilisimamiwa na Rais wa Ukraine Vlodomyr Zelensky.

    Aidha vyanzo hivyo katika kitengo hicho vimesema kwamba ndege zisizo na rubani za aina ya FPV vilivyotumiwa na kitengo hicho cha SBU zilirushwa angani na kufuatwa baadaye na majumba yaliyokwenye magurudumu yaliyotengenezwa kwa mbao.

    Pindi tu zilipoingia ndani ya himaya ya Urusi, ndege hizo zisizokuwa na rubani zilifichwa chini ya paa za majumba hayo yam bao na kuwekwa juu ya malori.

    Wakati wa shambulizi hilo, paa za majumba hayo zilifunguliwa kwa kutoka mbali na kuzipatia ndege zisizokuwa na rubani nafasi ya kupaa angani ten ana kulenga kambi za kijeshi za Urusi zilizokuwa karibu.

    Picha za video ambazo zimetolewa zinaonyesha ndege hizo zisizokuwa na rubani zikitoka kwenye paa ya mojawapo ya malori yaliyobeba majumba hayo yam bao.

    Ukraine inakadiria kwamba hasara iliyopatikana ni ya thamani ya dola bilioni 2 sawia na pauni bilioni 1.5.

    Ukraine ililenga kuharibu silaha aina ya TU -95 (ambayo ni silaha kubwa zaidi ya kurusha mabomu inayofahamika kama ‘Bear’ ), TU_22M3 (silaha inayorusha mabomu kwa masafa marefu) na A-50 ambayo ni ndege ya kutahadharisha majeshi mapema kwamba kuna tishio linalokaribia)

    Katika hatua nyingine, Mkuu wa jeshi la ardhini nchini Ukraine Jenerali Mkyhailo Drapatyi amejiuzulu, kutokana na shambulizi la kombora aina ya balistiki kutoka Urusi ambalo lililenga na kuharibu kambi ya mafunzo ya kijeshi ya Ukraine mapema Jumapili hii, ambapo wanajeshi 12 waliuawa.

  4. Habari za hivi punde, Shambulio kubwa la Ukraine nchini Urusi: Tunachojua kufikia sasa

    Kuhusu shambulio kubwa la ndege zisizo na rubani za Ukraine dhidi ya ndege za Urusi zilizolipuliwa.

    Hapa kuna muhtasari wa haraka wa kile tunachojua hadi sasa:

    • Idara ya usalama ya Ukraine inasema kuwa imeanzisha operesheni kubwa ya kuziangamizi kivita za kimkakati za Urusi.
    • Kampeni hii inalenga ndege za Urusi kwenye vituo vyao vya nyumbani - hadi sasa, Ukraine inasema imepiga maeneo 40 kama hayo, ikiwa ni pamoja na katika Arctic.
    • Video iliyotolewa na huduma inaonekana kuonyesha milipuko na moshi unaopanda

  5. Urusi yadai hujuma huku afisa mkuu wa jeshi la Ukraine akijiuzulu

    Hebu sasa tuangazie matukio mapya yaliyotokea Urusi na Ukraine katika saa chache zilizopita

    Wachunguzi kutoka Urusi wamesema kwamba kilichosababisha kuharibika na kuanguka kwa madaraja mawili tofauti karibu na mpaka wa Ukraine ni hujuma ambayo hawakutaja ilitekelezwa na nani.

    Katika jimbo la Bryansk, Daraja la Barabara lilianguka, na kusababisha malori makubwa kuangukia treni iliyokuwa imebeba abiria na kuwauwa watu saba.

    Picha hizi zinaonyesha jinsi mabogi ya treni hilo yalivyoharibiwa vibaya – Maafisa wa serikali wanasema kwamba abiria walisaidiana kuondoka kwenye treni hiyo iliyoharibiwa vibaya kukiwa na giza.

    Saa chache baadaye katika mji Jirani wa Kursk, Daraja lingine la reli lilianguka, wakati ambapo treni ya kubeba mizigo ilikuwa inapita juu, na kumjeruhi mmoja wa madereva wa treni hiyo.

    Kitengo cha ujasusi cha Jeshi la Ukraine kimesema kwamba treni ya jeshi la Urusi imeanguka katika mji wa Melitopol, kusini mwa Ukraine.

    Bila ya kutaja kwamba ni wao walihusika katika shambulizi hilo, kitengo hicho cha jeshi la Ukraine kimesema kwamba kilipuzi kililipuliwa wakati treni hiyo ilipita juu yake, na athari ilikuwa kubwa kwa kuwa treni hiyo ilikuwa imebeba mafuta na bidhaa ambazo zilikuwa zinasafirishwa hadi katika eneo ambalo Urusi inalikalia la Crimea.

    Katika dakika chache zilizopita, Kamanda wa jeshi la ardhini la Ukraine ametangaza kwamba anajiuzulu kazini, akitaja shambulizi hatari lililotekelezwa katika kambi ya mafunzo ya kijeshi ya Ukraine.

  6. Habari za hivi punde, Ukraine yazishambulia na kuziteketeza ndege 40 za kivita za Urusi

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Ukraine inadai kuzipiga takriban ndege 40 za Urusi 40, katika kile kinachoonekana kuwa moja ya mashambulizi makali zaidi hadi sasa kwenye anga za Urusi.

    Kulingana na taarifa kutoka kwa idara ya usalama ya Ukraine, SBU, "Ndege za kivita za kimkakati za adui zinateketea kwa wingi nchini Urusi ".

    Inasema Ukraine imeendesha "operesheni kubwa maalum inayolenga kuharibu ndege za adui."

    Inasema zaidi ya ndege 40 zimegongwa. Imetoa video ya kutisha ambayo inasema inaonyesha shambulio la ndege isiyo na rubani katika uwanja wa ndege wa Belaya katika mkoa wa Irkutsk, Siberia.

    Ndege za kivita zimeshambuliwa huku milipuko ikionekana na moshi ukiongezeka.

    Ripoti zinaonyesha kuwa ndege nyingine zimeshambuliwa katika uwanja wa ndege wa Olenya, karibu na Murmansk. Vyombo vya habari vya Urusi vinaripoti shambulio hilo huko Murmansk lakini vinasema ulinzi wa anga unafanya kazi. Shambulio la Irkutsk pia linaripotiwa.

    Wakati huo huo, mamlaka ya Ukraine inasema kuwa ndege zisizo na rubani 472 na makombora saba ya balistiki na ya cruise yalihusika katika wimbi la mashambulio ya usiku wa kuamkia jana dhidi ya Ukraine.

    Hili linaweza kuonekana kuwa shambulio moja kubwa zaidi la Urusi hadi sasa. Ukraine inasema ilipunguza malengo 385 ya angani.

  7. Hamas yatoa hakikisho la kuwaachilia mateka ila inataka mabadiliko kufanywa kwenye mpango wa kusitisha vita Gaza unaosimaiwa na Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Kundi la Hamas limejibu pendekezo la Marekani la kusitisha vita Gaza kwa kusema kwamba liko tayari kuwaachilia huru mateka 10 wa Israel walio hai na wengine 18 waliofariki katika mabadiliko yanayotakiwa kufanyika ambapo wafungwa kadhaa wa Kipalestina wanatarajiwa kuachiliwa huru.

    Aidha kundi hilo limesema kwamba lingetaka mabadiliko kadhaa kufanyiwa kwenye pendeekzo hilo kwanza.

    Kundi hilo lilisisitizia matakwa yake kwa ajili ya kupatikana kwa amani ya kudumu, likitaja kwamba lingetaka Israel kuondoka kabisa katika ukanda wa Gaza na hakikisho kwamba huduma za misaada zitaendelea bila kukatizwa.

    Kwa sasa masuala hayo hayako kwenye meza ya mazungumzo ya kusitisha vita Gaza.

    Hatua hii imesekama kwamba sio kukataa kabisa pendekezo la Marekani wala pia sio kukubaliana na pendeekzo hilo ambalo serikali ya Washington imesema Israel imekubaliana nalo.

    Hamas imesema kwamba imewasilisha majibu yake ya pendekezo la Marekani iliyowasilishwa na mjumbe maalum Steve WItkoff anayemuwakilisha rais Donald Trump katika eneo la mashariki ya kati.

    Katika taarifa WItkoff alisema kwamba: ‘Nimepokea majibu ya Hamas ya pendekezo la Marekani.

    Haikubaliki kabisa na ni jambo ambalo linaturejesha nyuma. Hamas inapaswa kukubali mfumo uliowekwa kwenye pendekezo hilo tulilowapa kwa misingi ya ukaribu wa mazungumzo ambayo yanatarajiwa kufanyika wiki hii, bila kuchelewa,’

    “ Hiyo ndio njia ya pekee ambayo tunaweza kukamilisha makubaliano ya kusitisha vita ya siku 60 katika siku chache zijazo.”

    Taarifa ya Waziri Mkuu wa israel imesema kwamba ;” Japo Israel imekubaliana na mabadiliko kwenye pendekezo lililowasilishwa na Bwana Witkoff ambayo inaweka wazi nanma mateka wa Israel watakavyoachiliwa, Hamas inazidi kushikilia msimamo wao wa kukataa pendekezo hilo.’

    Hamas ambalo ni kundi lililotangazwa kuwa kundi la kigaidi na Uingereza, Marekani na Umoja wa Ulaya EU, limesema kwamba linasisitiiza suala la “amani ya kudumu” na “kuondoka kabisa” kwa vikosi vya jeshi la Israel kutoka kwa ukanda wa Gaza.

    Kundi hilo limetaka msaada unaohitajika na wapalestina kuendelea kuingia katika ukanda huo uliozingirwa wa Gaza bila ya kusitishwa , na pia limesema kwamba mateka 10 walio hai na miili 18 ya mateka waliouawa ndio watakaobadilishana na wafungwa ambao idadi yao itakubaliana kati ya makundi hayo mawili.

    Ila Hamas inajipata katiak hali ngumu ambayo haijajipata tangu vita hivyo kuanza. Ikipata shinikizo kubwa, kutoka kwa watu milioni 2.2 wanaoishi katika eneo hilo na kupitia hali ngumu ya maisha.

    Kundi hilo linapokea pingamizi kubwa katika historia yake kutoka Gaza na kwa wanaosimamia mazungumzo ya amani, linapata ugumu kukubaliana na pendekezo la Marekani, ambalo kwa misingi tofauti linaonekana kuwa haliangazii mahitaji ya upande mmoja, na haliwezi kulinganishwa na pendekezo jinginezo la awalia ambalo pia ilkataa , hatua ya hivi punde ikiwa mwezi Machi.

  8. Raila Odinga ‘Walipeni fidia jamaa za waliofariki kwenye maandamano ya Gen Z 2024’

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Raila Odinga

    Kiongozi wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga amempongeza Rais William Ruto kwa kuliomba taifa msahama mapema wiki iliyopita katika kikao cha maombi ya kitaifa.

    Ila sasa anaitaka serikali nchini humo kufidia suala la maafa ya vijana katika maandamano ya kupinga mswada wa fedha 2024.

    Akizungumza katika sherehe za maadhimisho ya miaka 62 ya Madaraka, Raila ambaye kwa sasa ana ushirikiano wa karibu na Rais William Ruto amesema kwamba; ‘ Kuna vijana waliofariki Juni 25 2024 na wengine waliojeruhiwa, kuna haja ya serikali kutoa fidia kwa familia zao kama njia moja ya kutaka msamaha wa taifa pia.’ Alisema Odinga.

    Takriban vijana 60 walifariki mwaka jana kulingana na mamlaka ya kuchunguza shughuli za polisi IPOA ambayo inasema kwamba tayari kesi mbili za mauaji zinaendelea mahakamani ambapo polisi wanakabiliwa na mashitaka ya mauaji hayo.

    Kesi 22 kwa sasa zinaendelea kuchunguzwa huku IPOA ikisema kwamba hivi karibuni itatoa faili hizo na kuikabidhi ofisi ya mkurugenzi wa Mashtaka DPP kuwasilisha mahakamani.

    “Nimefurahi kwamba juzi Rais uliomba msahama kwa pamoja na Spika wa bunge la kitaifa n a hata Naibu wako, ila sasa kuna haja ya kuwaangalia vijana ambao walikuwa wanatetea haki yao,” alisema Odinga.

    Wengi wakati huo walimtaka Odinga kushiriki kwa pamoja na vijana kupinga mswada huo wa fedha wa 2024, huku akikosa kufiika barabarani kuandamana na vijana ambao kwa mwezi mzima walikabiliana na polisi barabarani .

    Kero la vijana lilizidi kuwa kubwa pindi tu bunge lilipopitisha mswada huo nayo matamshi ya baadhi ya wabunge kuashiria kwamba sauti ya vijana ilikuwa tu kelele za chura mtoni na wala hazingemzuia Ngombe kunywa maji.

  9. Mwanaharakati nchini Kenya azuiliwa kwa kubuni mtandao wa kupinga mswada wa fedha wa 2025.

    .

    Chanzo cha picha, Rose

    Wanaharakati nchini Kenya kwa pamoja na chama cha mawakili LSK wanaitaka idara ya polisi kumwachilia kwa dhamana ya polisi mwanaharakati Rose Njeri ambaye alikamatwa na anaendelea kuzuiliwa na polisi kwa kile LSK imekitaja shutuma ya kutengeneza mtandao wa maoni na kuwashawishi Wakenya wenzake kushiriki katika hatua ya kupinga mswada wa fedha 2025.

    Njeri ambaye ni mfanyabiashara na mtaalamu wa masuala ya fedha, alitumia ukurasa wake wa mtandao wa X kutoa mafunzo kwa Wakenya kuhusu yaliyomo kwenye mswada huo wa fedha 2025, ambao utajadiliwa bungeni mwezi huu baada ya Waziri wa fedha John Mbadi kusoma bajeti ya taifa mnamo Juni 12 mwaka huu.

    Kulingana na mwanaharakati Boniface Mwangi, wanaharakati wamepanga kuandamana hadi katika kituo cha polisi cha Pangani jijini Nairobi kuishinikiza polisi kumuachilia huru, kwa dhamana Njeri ambaye wanadai anaugua matatizo ya upungufu wa damu mwilini na anapaswa kupata lishe bora na matibabu.

    Siku ya Jumamosi, familia yake ilishinda katika kituo hicho ambapo wanadai kwamba afisa mkuu anayesimamia kituo hicho (OCS) aliwaeleza kwamba kesi hiyo inachunguzwa na idara ya uchunguzi wa jinai (DCI).

    Aliyekuwa Jaji Mkuu wa pili chini ya katiba mpya nchini Kenya David Maraga, amesema kwamba ,’ Vijnana nchini Kenya hawana cha kusherehekea katika siku kuu hii ya Madaraka kwa kuwa Uhuru wao unabanwa,’

    Aliendelea kusema kwamba, ‘Kukamatwa kwa Rose Njeri ni mfano wa hivi punde wa uongozi wa kiimla unoweka wazi kinaya katika siku hii ambapo taifa linasherehehea kujisimamia na kuangazia haki tulizonazo kidemokrasia.’

    Taarifa za kuwafahamisha wakenya kuhusu yanayopendekezwa katika mswada wa fedha 2025, zimeanza kuchapishwa katika mitandao ya kijamii huku wengi wakitumia X kueleza kero lao na mapendekezo yaliyomo kama vile madai kwamba VAT itapanda kutoka asilimia 16 hadi 18, na kwamba baadhi ya bidhaa ambazo zilikuwa zimekosa kutozwa ushuru kama vile maziwa na mkate, zingepanda bei katika hali ambayo wengi hawangeweza kukimu gharama yake.

    Wengi wanaitaka serikali kumuachia huru mwanaharakati huyo ambaye pia ni mtalaamu wa teknolojia ya kompyuta, wanasema kwamba kukamatwa kwakwe kunakiuka haki zake za kimsingi na ni shambulizi dhidi ya wanaojieleza kupitia mfumo wa kidijitali.

    Mwaka mmoja uliopita, Vijana nchini Kenya waliandamana kupinga mswada wa fedha 2024 ambao walihisi ulikuwa unambana Mkenya zaidi na ungepandisha hali ya maisha ambayo wengi hawangeweza kukimu mahitaji yao ya kila siku.

    Msururu wa maandamano yaliendelea kwa wiki kadhaa hadi Juni 25 ambapo mambo yaligeuka kuwa magumu vijana walipolivamia bunge la Kenya huku polisi wakiwafyatulia risasi.

    Baada ya ghasia za saa kadhaa vijana kadhaa walifariki, huku wengine wengi wakiripotiwa kukamatwa katika hali tatanishi na kupotea kwa muda.

    Wengi waliojaribu kuikashifu serikali kupitia taarifa mitandanoni walipotea na baada ya kupatikana walikuwa katika hali mbaya ya kiafya na kiakili.

    Rais WIllliam Ruto alikanusha madai kwamba polisi wanawakamata raia, ila wiki chache zilizopita alisema kwamba wote walioripotiwa kupotea walirejeshwa makwao. Ila baadhi ya familia bado zinasema kwamba wana wao hadi sasa hawajulikani walipo.

    Kumhusu Rose Njeri, Rais wa LSK Faith Odhiambo amesema kwamba mawakili watafika mahakamani Jumanne wiki hii kuishinikiza serikali kumfikisha kortini au kuachilia huru mwanaharakati huyo akilalamikia alivyozuiliwa bila ya mawakili wake kupata fursa ya kumuona au kupata dhamana ya polisi.

    .

    Chanzo cha picha, X

  10. Mamia wakamatwa kwenye ghasia zilizotokea Paris baada ya ushindi wa PSG wa klabu

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    PICHA: magari yalitekekezwa moto wakati wa ghasia zilizotokea baada ya klabu ya PSG kushinda kombe la UCL ambalo ni kubwa zaidi kwa klabu hiyo kuhsinda.

    Mamia ya watu wamekamatwa jijini Paris, Ufaransa kutokana na makabiliano kati ya mashabiki wa klabu ya Paris Saint-Germain (PSG) waliokuwa wakisherehekea ushindi wa klabu hiyo katika michuanooya fainali ya kombe la klabu bingwa ulaya UCL.

    Polisi waliwakamata watu 300 baada ya ghasia kuzuka karibu na Barabara ya Champs – Elysees iliyopo karibu na uwanja wa klabu hiyo ambapo PSG iliicharaza Inter Milan mabao 5 -0 .

    Moto iliwashwa pamoja na fataki, huku maeneo ya kusubiria mabasi yaivamiwa na kuharibiwa, huku magari yakitekeketzwa moto wakati wa sherehe hizo ambazo polisi wanasema zilipitiliza hali ya usalama.

    Ghasia izlizuka baada ya PSG kushinda kombe hilo kubwa katika soka ya bara ulaya kwa mara ya kwanza katika historia ya klabu hiyo.

    Mashabiki wengi walisherehekea kwa ustaarabu huku baadhi wakiimba na kucheza kwenye Barabara za Paris au wakicheza muziki kwa suati kubwa kwenye magari yao.

    Mnara wa Eiffel Tower ulikuwa na mwanga wa rangi za timu hiyo za samawati na nyekundu, huku Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ambaye ni shabiki mkubwa wa klabu ya Olympique Marseille akiipongeza klabu hiyo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa X:

    ‘Ni siku njema kwa PSG! Hongera, tunajivunia ushindi wao. Paris ambayo ni makao makuu ya bara ulaya kwa usiku huu.’

    Takriban polisi 5,400 walikuwa wanashika doria kote Paris wakiwa wamejiandaa kwa lolote kutokea katika sherehe za ushindi huo wa PSG.

  11. Watu saba wafariki baada ya madaraja mawili ya Urusi kuporomoka

    .

    Chanzo cha picha, Moscow Interregional Transport Prosecutor's Office

    Madaraja mawili yameporomoka usiku kucha katika matukio tofauti katika mikoa ya Urusi inayopakana na Ukraine, na kuua takriban watu saba na wengine kadhaa kujeruhiwa. Huduma za dharura zilisema takriban watu saba waliuawa.

    Takriban watu 47 walipelekwa hospitalini, akiwemo mtoto mmoja, Gavana Alexander Bogomaz alisema. Reli ya Moscow ilidai kwenye Telegram kwamba daraja hilo lilianguka kwa sababu ya "uingiliaji haramu".

    Saa chache baadaye daraja la pili liliporomoka katika wilaya ya Zheleznogorsk, na kuacha treni kukosa mwelekeo - kaimu gavana Alexander Khinshtein alisema.

  12. Wakenya washerehekea sikukuu ya Madaraka Day

    Rais wa Kenya William Ruto kwa sasa anaongoza sherehe za siku kuu ya Madaraka Day nchini Kenya ambazo zinaandaliwa katika uwanja wa Raila Odinga uliopo kaunti ya Homa Bay magharibi wa taifa hilo.

    Maadhimisho hayo ya 62 ya uongozi wa Madaraka na uongozi wa Wakenya yanaadaliwa wakati ambapo taifa linakumbana na changamoto za ukosefu wa ajira kwa vijana, hali ngumu ya kiuchumi licha ya sarafu ya Kenya kustawi dhidi ya sarafu ya dola ya Kimarekani, na vile vile malalmishi ya hasa vijana kuhusiana na jinsi taifa linavyoendelea mbele.

    Rais William Ruto – Rais wa awamu ya tano, amesisitiza kwamba analiongozoa jahazi la Kenya kwa uthabiti, japo wengi nchini wanahisi kwamba kuna mambo mengi ambayo hayasimamiwi vyema.

    Kwa sasa madaktari wa mfummo wa afya wa UHC {Universal Health Coverage} wanagoma katika baadhi ya kaunti nchini Kenya, huku wengi wakilalamikia bima mpya ya malipo ya matibabu ya SHA ambayo wanahisi haijaanza kushughulikia wagonjwa ipasavya.

    Usalama katika maeneo ya mipakani umekuwa tatizo kutokana na mashambulizi ya kundi la Al sha baab huku wengi wakihisi kwamba ahadi za mzee Jomo Kenyatta mwaka wa 1964 Kenya ilipojipatia uhuru wa kujisimamia bado hayajatimizwa.

    Wakati huo Mzee Kenyatta akipokezwa mamlaka ya kuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Kenya .

  13. Watu 26 wafariki baada ya vifaru vya Israel kushambulia Gaza - waokoaji

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Takriban watu 26 wameuawa, na wengine kadhaa wamejeruhiwa, karibu na kituo cha kusambaza misaada kinachoungwa mkono na Marekani karibu na mji wa kusini wa Gaza wa Rafah, kulingana na matabibu na wakaazi.

    Mwandishi wa habari wa Palestina aliiambia BBC kuwa maelfu ya Wapalestina walikuwa wamekusanyika karibu na kituo cha kusambaza misaada ya kibinadamu wakati vifaru vya Israel vilipokaribia na kuufyatulia risasi umati huo.

    Tukio hilo limeripotiwa kutokea magharibi mwa Rafah, kusini mwa Ukanda wa Gaza, na waliojeruhiwa wanatibiwa katika moja ya hospitali chache zinazofanya kazi Gaza huko Khan Younis.

    Haya yanajiri huku Marekani ikijaribu kusuluhisha usitishaji mapigano na Israel ikikabiliwa na ukosoaji wa kimataifa kuhusu hali ya kibinadamu huko Gaza.

    Tutakuletea zaidi kuhusu hili na maendeleo ya hivi punde katika vita, kaa nasi.

  14. Natumai hujambo na karibu katika habari zetu za moja kwa moja